Nasoro Mchunga, mwanafunzi wa kozi ya Music and Sound Production katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa), ameendelea kuonesha umahiri wake katika sanaa ya ushairi, kipaji ambacho anasema alianza kukiendeleza mwaka 2020 alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha kwanza.Nasoro anabainisha kuwa mapenzi yake kwa ushairi yalianza tangu akiwa shuleni, ambapo alianza kutunga mashairi mbalimbali yaliyolenga kuelimisha, kuburudisha na kuhamasisha jamii kuhusu masuala tofauti ya kijamii.Amewahimiza vijana wenye vipaji mbalimbali kuviendeleza kwa kujituma, kujifunza na kutokata tamaa, akisisitiza kuwa vipaji vinaweza kuwa daraja la kufikia mafanikio makubwa endapo vitapewa nafasi ya kukuzwa.
Mkazi wa Bagamoyo, Bw. Shabani Ramadhani, ameeleza kuwa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) imekuwa na mchango mkubwa katika kukuza, kuendeleza na kutangaza sanaa nchini Tanzania kwa miaka mingi.Amesema uwepo wa TaSUBa umeiwezesha Bagamoyo kuwa kitovu muhimu cha sanaa na utamaduni, huku ikitoa fursa kwa vijana wengi kupata elimu ya sanaa na kuendeleza vipaji vyao katika nyanja mbalimbali za ubunifu.Bw. Ramadhani pia amepongeza Tamasha la Kimataifa la Sanaa na Utamaduni Bagamoyo, akieleza kuwa tamasha hilo limekuwa jukwaa muhimu linalowakutanisha wasanii kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali duniani kwa ajili ya kubadilishana uzoefu, kuonesha kazi zao na kuimarisha ushirikiano wa kiutamaduni.
Mwalimu Felix Sesoa ambaye ni mkufunzi katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) anaeleza kuwa teknolojia ya majukwaa (Stage Technology) ni sehemu muhimu katika mafanikio ya maonesho yoyote ya sanaa, kwani huchangia kwa kiasi kikubwa ubora wa uwasilishaji wa kazi za wasanii kwa hadhira.Anaeleza kuwa teknolojia ya majukwaa inahusisha matumizi ya vifaa na mifumo mbalimbali ya taa, sauti, mapambo ya jukwaa, pamoja na mbinu za kiufundi zinazowezesha maonesho kufanyika kwa ufanisi na kuvutia watazamaji."Hata kama wasanii wana vipaji vikubwa, maonesho yao yanaweza kupungua thamani endapo hayatasaidiwa na teknolojia bora ya jukwaani," anasema Mwl. Sesoa.
Copyright ©2024 Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) . All rights reserved.