MKUFUNZI katika Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa), Bi. Beatrice Taisamo, amesema kuwa nidhamu katika kazi ni moja ya nguzo muhimu zinazo mwezesha msanii kukua kitaaluma na kuzalisha kazi zenye ubora unaokubalika.Akizungumza kuhusu safari yake ya sanaa, Bi. Taisamo alieleza kuwa msanii mwenye nidhamu huipa kazi yake muda, heshima na nguvu zote zinazohitajika ili kufikia malengo aliyojiwekea. Anaongeza kuwa nidhamu humsaidia msanii kushirikiana vyema na wenzake, jambo ambalo huongeza ufanisi na mafanikio katika kazi za pamoja.Bi. Taisamo pia alibainisha kuwa aliamua kujiunga na TaSUBa kwa lengo la kunoa na kukuza kipaji chake cha uigizaji baada ya kugundua kuwa alikuwa na uwezo mkubwa katika sanaa hiyo. Kupitia mafunzo aliyoyapata chuoni hapo, ameweza kuimarisha ujuzi wake na hatimaye kuwa miongoni mwa walimu wanaochangia kuibua na kuendeleza vipaji vya wasanii chipukizi nchini.
Meneja wa Msanii Alikiba na Meneja wa Kings Music Records, Bw. Benjamin Otwal, amewahimiza vijana kuzingatia “creative economy” kama njia muhimu ya kujenga maisha bora ya baadaye na kufikia mafanikio katika sekta ya sanaa na ubunifu.Akizungumza na wanachuo wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa), Bw. Otwal amesema kuwa dunia ya sasa inahitaji vijana wenye uwezo wa kutumia vipaji vyao kwa ubunifu ili kujiongezea kipato na kuchangia maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.Amesema TaSUBa ni miongoni mwa taasisi zinazotoa mazingira bora ya kujifunzia na kukuza vipaji vya kisanaa kwa kuwaunganisha wanafunzi na wataalamu wa sekta mbalimbali za sanaa na ubunifu.
Wanachuo wa Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) wamepata semina maalum iliyotolewa na Rais Mstaafu wa Shirikisho la Filamu Tanzania Bw. Eliya Mjatta, iliyolenga kuwajengea uwezo wa kubadili vipaji vyao vya kisanaa kuwa chanzo endelevu cha kipato na maendeleo ya kiuchumi.Akizungumza katika semina hiyo, mwezeshaji huyo aliwahimiza wanafunzi kuondokana na mtazamo wa kuona sanaa kama kipaji pekee na badala yake kuichukulia kama biashara yenye uwezo wa kuzalisha ajira, kipato na fursa mbalimbali za maendeleo.Alieleza kuwa mafanikio katika sekta ya sanaa yanahitaji ubunifu unaoambatana na fikra za kibiashara, ikiwa ni pamoja na kutambua mahitaji ya soko, kujitangaza kitaalamu, kujenga mitandao ya kikazi na kuwekeza katika ujuzi unaoongeza thamani ya kazi zao.
Copyright ©2024 Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo (TaSUBa) . All rights reserved.